BENO KAKOLANYA ANYOOSHA MIKONO KWA KASEJA

KIPA wa timu ya Yanga, Benno Kakolanya, amempigia saluti mlinda mlango wa KMC, Juma Kaseja, kutokana na kazi kubwa aliyoifanya juzi akiwa langoni katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

Yanga sasa wanashika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu, baada ya juzi kufanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya KMC katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Akizungumza na BINGWA jana, Kakolanya alisema siku zote mchezo unakuwa mgumu kwa kipa kwa kuwa akili na nguvu ya kila mchezaji inawaza kuliona lango na hilo linawapa kibarua kizito kuhakikisha nyavu hazitikisiki.

Alisema Kaseja amefanya kazi kubwa na hata bao alilofungwa halikuwa la kizembe kwa sababu upande wake ulikuwa unashambuliwa zaidi kuliko kwake, ingawa walikuja kupata bao dakika za mwishoni, jambo ambalo wanajivunia.

“Kaseja ni kipa mzuri anayejua kupambana, hata lile bao alilofungwa juzi kama kuna wanaomlaumu hawajui mpira, maana kazi aliyoifanya akiwa langoni ni kubwa,” alisema.

Hata hivyo, Kakolanya alisema kwa upande wake, yupo kwa ajili ya kuipigania timu yake akiwa kama tegemeo la mwisho, kwani iwapo wapinzani watawazidi maarifa, mabeki yeye ndiyo mtu pekee anayetakiwa kuinusuru timu.

Pia aliongeza kuwa hana hofu na kikosi hicho  kwa sasa, kwani kinafanya vizuri na pia watahakikisha kasi inaendelea ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa msimu huu

LihatTutupKomentar