MBWANA SAMATTA AENDELEZA UBABE GENK

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta leo ameifungia bao pekee timu yake, KRC Genk ikiibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Anderlecht katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji Uwanja wa  Luminus Arena mjini Genk.
Samatta ambaye ni Nahodha wa Taifa Stars alifunga bao hilo dakika ya 54 akimalizia pasi ya mshambuliaji mwenzake, Mjapan Junya Ito.
Hilo linakuwa bao la nne kwa Samatta msimu huu, baada ya kufunga mabao matatu peke yake katika ushindi wa 4-0 dhidi ya Waasland-Beveren.


Mbwana Samatta amefunga bao lake la nne la msimu leo Genk ikishinda 1-0 dhidi ya Anderlecht

Pamoja na ushindi huo, Genk inabaki nafasi ya tano ikiwa na pointi tisa baada ya kucheza mechi tano, imefungwa mbili na kushinda tatu. Inalingana na Standard Liege na Antwerp na inazidiwa pointi moja moja na Club Brugge na Mechelen, ambazo hata hivyo zite zimecheza mechi nne kila moja.
Kwa Samatta mwenye umri wa miaka 26 leo amefikisha mabao 67 ya kufunga katika mechi ya 161 za mashindano yote tangu amejiunga na KRC Genk Januari mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Katika ligi ya Ubelgiji pekee amefunga mabao 52 kwenye mechi 127, kwenye Kombe la Ubelgiji amecheza mechi tisa na kufunga mabao mawili, katika Super Cup mechi moja na Europa League mechi 24 katika mabao 14.
Kikosi cha KRC Genk kilikuwa; Coucke, De Norre, Dewaest, Lucumi, Uronen, Heynen, Berge, Piotrowski/Hrosovsky dk73, Ito, Paintsil/Ndongala dk89 na Samatta.
RSC Anderlecht; Van Crombrugge, Kompany/Cobbaut dk77, Vlap, Nasri, Chadli/Adzic dk73, Zulj, Sandler/Kana dk70, Amuzu, Dewaele, Verschaeren na Sardella

LihatTutupKomentar