YONDANI AKUTANA NA FIFA


BEKI wa kati wa Yanga, Kelvin Yondani, juzi alijikuta katika mikono ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), alipotakiwa kupimwa iwapo anatumia dawa za kuongeza nguvu zilizokatazwa
na Shirikisho hilo.
Tukio hilo lilitokea baada ya mchezo wa pili wa Yanga wa hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Rayon Sports ya Rwanda, kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, ulioishia kwa timu hizo kutoka suluhu.
Mbali ya Yondani, wachezaji wengine waliopimwa ni mshambuliaji wa Yanga, Yohana Nkomola na nyota wa Rayon, Pierre Kwizera na Muhire Kevin.
Ni utamaduni wa Fifa kuwapima wachezaji iwapo wanatumia dawa zilizokatazwa michezoni, ili kukomesha vitendo hivyo ambavyo vilishaanza kukithiri. Mara baada ya mchezo huo, wachezaji hao
walichukuliwa na kuingizwa kwenye chumba cha madaktari na kufanyiwa vipimo hivyo.
Mchakato wa tukio hilo uliongozwa na mwakilishi mmoja kutoka FIFA, aliyewataka madaktari wa timu zote mbili kwenda katika chumba hicho na kuokota vikaratasi viwili kati ya 18 vilivyoandikwa namba za jezi za wachezaji wa Yanga na Rayon. Hapo ndipo majina ya wachezaji hao
yalivyopatikana na kufanyiwa vipimo hivyo.
Akizungumzia tukio hilo, daktari wa Yanga, Edward Bavu, alisema tukio hilo ni la kawaida na si geni kwa timu yao, kwani hata mwaka jana katika hatua ya makundi wa michuano hiyo, wachezaji wao wawili, Juma Abdul na Donald Ngoma, walichukuliwa kipimo hicho.
LihatTutupKomentar